IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika kikao cha Mkuu wa Idara ya Mahakama ya Iran

Kusimama kidete mbele ya maadui ni siri ya maendeleo ya Jamhuri ya Kiislamu

18:24 - June 28, 2022
Habari ID: 3475438
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amehutubia kikao cha Mkuu wa Idara ya Mahakama ya Iran na maafisa na wafanyakazi wa chombo hicho akisema matokeo ya kusimama kidete mbele ya maadui ni kupata ushindi na maendeleo.

Katika kikao hicho, Ayatullah Ali Khamenei amefafanua kanuni zisizobadilika za Mwenyezi Mungu katika jamii na kusema: Sababu ya ushindi wa kustaajabisha wa taifa la Iran na Jamhuri ya Kiislamu katika matukio makubwa na machungu ya mwaka 1360 (Hijria Shamsia) ni mapambano, juhudi na kutowaogopa maadui, na kanuni hiyo ya Mwenyezi Mungu inaweza kukaririwa katika vipindi na zama zote; hivyo inatupasa kufahamu kuwa Mwenyezi Mungu wa mwaka huu wa 1401 Ndiye Yuleyule wa mwaka 1360. 

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria mifano ya kanuni na sheria za Mwenyezi Mungu ndani ya Qur'ani kuhusiana na matokeo ya kuinusuru dini ya Mwenyezi Mungu au matokeo ya kukufuru neema Zake SW na kuongeza kuwa: Qur'ani Tukufu imejaa Aya zinazohusiana na kanuni za Mwenyezi Mungu, na hitimisho la Aya hizo ni kwamba ikiwa jamii zitasimama kidete dhidi ya maadui na kutekeleza majukumu yao kwa kumtegemea Mwenyezi Mungu, matokeo yake ni ushindi na maendeleo; lakini iwapo zitakumbwa na hitilafu, kuzama katika anasa na udhaifu, matokeo yake yatakuwa kushindwa.

Ayatullah Khamenei amezungumzia jinsi adui alivyofurahia kutokana  na baadhi ya udhaifu na mapungufu ya ndani katika baadhi ya vipindi, na akasema: "Katika mwaka 1360 (Hijria Shamsia) na baada ya hapo katika miongo minne iliyopita, adui alifurahi na kupata matumaini katika baadhi ya matukio na akadhani kwamba Mapinduzi na Mfumo wa Kiislamu umo katika hali ya kuporomoka, lakini matumaini hayo yamegeuka na kuwa hali ya kukata tamaa; tatizo lao ni kwamba hawaelewi siri ya kukata tamaa huko."

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi amesisitiza kuwa: Adui hawezi kuelewa kwamba katika ulimwengu huu, mbali na hesabu za kisiasa, kuna mahesabu mengine ambayo ni kanuni za Mwenyezi Mungu.

4067211

captcha