Kwa mujibu wa kitengo cha habari cha Ofisi ya Kiongozi Muadhamu, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amezuru haram tukufu ya Imam Khomeini (MA) na kaburi la mwana na kumbukumbu ya mwasisi huyo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kuwapigia faatiha.
Ayatullah Khamenei amezuru pia makaburi ya Mashahidi 72 wa tukio la kigaidi la tarehe 7 Tir na Mashahidi wa mripuko uliotokea ndani ya ofisi ya Waziri Mkuu mwaka 1980 na kuenzi kumbukumbu za Mashahidi Beheshti, Rajaei, Bahonar na wenzao waliouawa shahidi pamoja nao.
Vilevile Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amezuru makaburi ya Mashahidi adhimu wa Mapinduzi ya Kiislamu, wa vita vya miaka minane vya Kujihami Kutakatifu na wa ulinzi wa Haram tukufu ya Bibi Zainab (SA).
Mapinduzi ya Kiislamu yalifikia kwenye ushindi tarehe 11 Februari 1979 kwa uongozi wa mwanachuoni shujaa, Imam Khomeini Mwenyezi Mungu Amrehemu.
Siku ya kurejea kwa Imam Khomeini nchini Iran (Februari 1) ni mwanzo wa Siku Kumi za Fajr (Siku Kumi za Alfajiri), ambazo hufikia kilele kwa mikusanyiko ya kumbukumbu ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu tarehe 11 Februari.
Taifa la Iran liliupindua utawala wa Pahlavi unaoungwa mkono na Marekani miaka 45 iliyopita, na hivyo kuhitimisha miaka 2,500 ya utawala wa kifalme nchini humo.
Mapinduzi ya Kiislamu yaliyoongozwa na hayati Imam Khomeini yalianzisha mfumo mpya wa kisiasa unaozingatia maadili na demokrasia ya Kiislamu.
3487034