Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, wanawake 19 kutoka Iran na nchi mbali mbali duniani wameenziwa na kutunukiwa zawadi katika Duruy a Sita ya Kuwaenzi Wanawake Wasomi wa Qur'ani.
Kati ya walioenziwa ni Munia Al Alami Qarshi wa Tunisia ambaye ni mtafiti, mhadhiri msaidizi katika chuo kikuu na muhubiri katika televisheni nchini Tunisia, Basma Bint Mohammad bin Khalfan al Al Bassami wa Oman ambaye ni mratibu wa mipango ya Qur;ani katika Taasisi na Madrassah ya Qur;ani nchini Oman. Halikadhalika ameenziwa Haura Ali Abdullah kutoka Lebanon ambaye ni mwanachuo wa Shahada ya Uzamili (MA) katika Sayansi za Qur'ani na pia mwandishi vitabu vya kidini mbali na kuwa mwalimu wa Qur'ani nchini Lebanon.
Halikadhalika ameenziwa Dardane Ja'afari kutoka Jamhuri ya Azerbaijan ambaye ni mtarjumi wa Qur'ani Tukufu kwa lugha ya Kiazeri. Wengine waliotunukiwa zawadi katika hafla hiyo ni Iman Louis kutoka Indonesia ambaye ni mhadhiri wa sayansi za Qur'ani katika Chuo Kikuu na mwingine alikuwa Hannan Kadhim kutoka Iraq ambaye ni jaji katika mashindano ya Qur'ani mbali na kuwa mwalimu wa Qur'ani, qarii na hafidh wa Qur'ani Tukufu.
Awamu ya 32 ya Mashindano ya Kimataifa ya Qur'ani Tukufu ya Iran yalianza Ijumaa Mei 15 (27 Rajab) kwa mnasaba wa kubaathiwa Mtume SAW. Mashindano hayo ya wiki moja yamewaleta pamoja maqarii 120 kutoka nchi 75.../mh