Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, Hijabu hiyo maalumu ya wanamichezo Waislamu imekuwa ikitayarishwa kwa muda wa maka moja na hata imefanyiwa majaribio na wanamichezo wanawake Waislamu akiwemo mchezaji skate Bi. Zahra Lari.
Hijabu hiyo imetengenezwa kwa kitambaa chepesi chenye kujivuta na ambacho kina mashimo madogo sana ili kuwezesha hewa kuingia na kutoka kwa urahisi. Hijabu hiyo imezinduliwa kwa rangi tatu na inatazamiwa kuanza kuuzwa mwaka 2018.
Lari, ambaye atashiriki katika Mashindano ya Olimpiki ya Msimu wa Baridi huko Pyeongchang, Korea Kusini, mwakani ametuma picha katika mtandao wake wa kijamii wa Instagram akiwa amevalia Hijabu hiyo ya Nike. Lari ambaye ni mkaazi wa Abu Dhabi anayewakilisha Umoja wa Falme za Kiarabu ameandika chini ya picha hiyo kuwa, "siamini kuwa hatimaye imefika."
Katika mashindano ya Olympiki huko Rio nchini Brazil mwaka jana, Ibtihaj Muhammad wa New York alikuwa mwanamke wa kwanza Mmarekani kuiwakilisha nchi yake katika Olimpiki akiwa amevaa Hijabu.
Agosti mwaka 2010, Shirikisho la Soka Duniani FIFA limeiruhusu Timu ya Taifa ya Soka ya Vijana wa Kike ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kushiiriki katika mashindano ya Olympiki ya Vijana nchini Singapore wakiwa wamevaa sare za kike zinazoenda sambamba na mafundisho ya Kiislamu.
3462369