Katika taarifa, Al Azhar imesema kitendo cha wanachama wa chama tawala cha India cha Bharatiya Janata (BJP) ni ishara ya ujahilia na ujinga wao kuhusu historia na Sirah ya Mtume Muhammad SAW.
Aidha Al Azhar imesema matamshi hayo yenye kuvunjia heshima matukufu ya dini yatachochea misimamo mikali ya kidini na kueneza chuki baina ya wafuasi wa dini mbali mbali. Halikadhalika Al Azhar imesema matamshi ya kumvunjia heshima Mtume Muhammad SAW ni mfano wa wazi wa ugaidi halisi ambao unaweza kuitumbukiza dunia katika migororo na vita na kwa msingi huo dunia inapaswa kuchukua hatua za kivitendo kuzuia matamshi kama hayo.
Katika matamshi ya hivi karibuni katika mdahalo wa televisheni, msemaji wa BJP Nupur Sharma alitoa matamshi ya kichochezi dhidi ya Mtume wa Uislamu, ambayo yamelaaniwa kote India na kuibua ghasia katika jimbo la Uttar Pradesh Kanpur siku ya Ijumaa. Jana Jumapili chama cha BJP kilitangaza kusimamisha uanachama wa Sharma na kujiweka mbali na matamshi yake yenye chuki.
Aidha chama hicho kimemfukuza Naveen Kumar Jindal ambaye anasismamia kitengo cha habari cha chama hicho mjini New Delhi ambaye alituma ujumbe uliomvunjia heshima Mtume Muhammad SAW katika ukurasa wake wa Twitter na kufuatia malalamiko alifuta ujumbe huo.
Nchi za Kiislamu ambazo zimelaani kauli za kumvunjia heshima Mtume SAW nchini India ni Iran, Indonesia, Malaysia, Qatar, Kuwait na Jumuiya ya Ushirikiano wa Nchi za Kiislamu (OIC).